Familia yaomba serikali kuwasaidia kutoa mwanao anayeteseka Saudia
Familia ya Francina Magati, 39 imeomba serikali ya Kenya kuingilia kati na kuwasaidia kumtoa mwanao anayeteseka Saudi Arabia alipoenda kufanya kazi.
Kupitia kwa mamake mwathiriwa Terezi Mueni,familia hiyo ilisema binti yao anateswa kwa kulazimishwa kufanya kazi licha ya kuwa ni mgonjwa na juhudi zake za kutafuta matibabu hazijafua dafu.Vilevile,bintiye hajapokea dawa na chakula ikiwemo kulipwa mshahara .
“Alifikishwa hospitalini,daktari akasema hawezi fanya kazi,waajiri wakakata.Aliwalilia (waajiri) hawezi kazi wamrudishe Kenya akatibiwe lakini wakakata.Maajenti walimuuza tena kwa mwajiri mwingine,” alisema mamake Francina.
Mamake mwathiriwa amewashutumu maajenti kwa kuwa kizingiti kwa mwanao kupata kibali cha kurudi nchini kutoka ubalozi wa Saudia hata alipoomba kuwakabidhi fedha za kumkatia tiketi ya kurudi Kenya ombi lake halijakubaliwa.
“Mzee Swaleh kwenye ubalozi alianza kumtandika,alimpigia hadi wenzake wakanipigia simu kuniambia mwanangu anaumia sababu katetea haki yake,” alisema mama Mueni.
“Kila mara akitafuta muhuri kwa stakabadhi zake ripoti inaenda kwa mama anaitwa Fatuma anayesema asipatiwe ruhusa,ateseke.Amemtukana sana,” akaongezea.
kupitia kwa afisa anayeshughulikia masuala ya dharura katika Shirika la kutetea haki za binadamu la Haki Afrika Mathias Shipeta alikashifu kitendo hicho akisema ni ukiukaji wa haki za binadamu na kurai serikali ya Kenya na ubalozi wa Saudia kuingilia kati na kumsaidia mwathiriwa.
Shipeta ameongezea kuwa ada wanayopata maajenti wanaosafirisha wasichana nje ya nchi kikazi inafanya vigumu kwa maajenti hao kusaidia waathiriwa licha ya kuwa haki zao zinakiukwa.